Pages

Ads 468x60px

Saturday, May 19, 2012

WAFANYA BIASHRA NDOGONDOGO (MACHINGA) WAKIENDELEA NA BIASHARA ZAO MAENEO YA UHINDINI JIJINI MBEYA.

NAO WANUNUZI WANAENDELEA KUPATA HUDUMA HII YA WAMACHINGA KATIKA MAENEO YA UHINDINI JIJINI MBEYA.
XXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXX

-JIJI LA KIRI  WAMACHINGA KUTOVAMIA MAENEO.
 
-WAPO KWA MUDA WAKATI SERIKALI IKIKAMILISHA MAENEO WALIYOTENGEWA.
-WAMACHINGA  WASEMA TUPO TAYARI KUHAMIA MAENEO MAPYA
 
HALMASHAURI  ya Jiji la Mbeya, imesema wafanyabiashara ndogondogo maharufu kwa jina la (Wamachinga) hawajavamia maeneo wanayofanyia biashara zao sasa  bali wapo kwa muda wakati serikali ikikamilisha miundombinu kwenye maeneo waliyoyapendekeza.
 
Wamachinga hao ni wale wanaoendeshea biashara zao kandokando ya barabara inayoingia kwenye soko kuu la Mwanjelwa pamoja na wale wa barabara inayoanzia eneo la Mafiat kuelekea Soko Matola.
 
Awali, halmashauri ya Jiji la Mbeya, iliwaondoa wa machinga bila ya kuwashirikisha  jambo lililopelekea wafanyabiashara  hao kufanya vurugu zilizoambatana na  kufunga barabara katika eneo la Mwanjelwa, wakipinga kuondolewa katika eneo wanalofanyia biashara zao ndogondogo bila kuoneshwa eneo jipya.
 
Akizungumza na Freedonia Leo kwa njia ya simu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Mbeya, Juma Iddy alikiri kuwepo kwa wamachinga kwenye maeneo yasiyoruhusiwa na kwamba wapo kwa muda wakati wakisubili kukamilishwa kwa eneo maalumu walilotengewa.
 
“Wamachinga hawajarudi, wapo kwa muda wakati serikali ikikamilisha baadhi ya miundombinu kwenye maeneo mapya na ifikapo Mei 30  mwaka huu maeneo hayo yatakuwa yamekamilika,” alisema
 
Aliyataja maeneo hayo kuwa ni eneo la barabara ya Bulongwa-iliyopo nyuma ya Soko jipya Mwanjelwa, eneo la Chuo cha wafanyakazi(OTTU) pamoja na eneo   Moondust-Soweto.
 
 Aidha, Iddy alifafanua kuwa ifikapo Juni 15, mwaka huu wamachinga hao watatakiwa kuhamia kwenye maeneo hayo na endapo watakaidi agizo hilo hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi yao.
 
Wamachinga kwa upande wao walisema, wapo tayari kuondoka kwenye barabara hizo endapo serikali itawapeleka kwenye maeneo ambayo wameyapendekeza.
 
“Tupo tayari kuondoka kwenye eneo hili la barabara kama serikali itafuata mapendekezo yetu  kuhusu eneo tunalolihitaji,”alisema John Kadege
 
Alisema, moja ya eneo walilolipendekeza ni kandokando ya Benki ya Posta mbali na lile walilopatiwa wahanga wa moto wa soko kuu la Uhindini.
 
Freedonia Leo, lilifanikiwa kuzungumza na mmoja wa wanunuzi wa bidhaa hizo zilizotandazwa kandokando ya barabara Alex Sichale, alisema kitendo cha wafanyabiashara hao kuendesha biashara kandokando ya barabara ni ukiukwaji wa sheria pia ni usumbufu kwa wapita njia pamoja na waendesha magari.
 
 
Akizungumzia suala hilo Diwani wa Kata ya Forest Boyd Mwabulanga kupitia chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), alisema wamachinga wanatakiwa kutii na kutekeleza sheria mbalimbali ikiwemo ya uendeshaji wa biashara katika maeneo maalumu.
 
“Halmashauri ipo katika hatua za mwisho za  ukarabati wa miundombinu katika maeneo yaliyopendekezwa na wamachinga wenyewe hivyo watakapotakiwa kuondoka basi kusiwepo na siasa,”alisema
 
Freedonia Leo, lilifanikiwa kuzungumza na Diwani  wa Kata ya Itezi  Frank Mahemba kupitia chama cha mapinduzi(CCM) ambaye alisema mzungumzaji wa suala hilo ni Meya wa Jiji la Mbeya.
 
Jitihada za kumpata Mstahiki Meya wa Jiji la Mbeya Athanas Kapunga zilishindikana baada ya kumkosa ofisini na alipotafutwa kwa njia ya simu hakupatikana.
 
Mwisho.

0 comments:

Post a Comment