(Picha zote na Benedict Liwenga)
Na. Jacquiline Mrisho.
Katibu Mkuu wa Shirikisho la Vyama
Huru vya Wafanyakazi (TUCTA) amezisifia sheria za kazi kwa kuwa zimesaidia
kuleta mabadiliko katika Nyanja za utoaji wa haki kazini.
Hayo yamesemwa leo na Katibu Mkuu wa Shirikisho
la Vyama Huru vya Wafanyakazi Nicholaus Mgaya wakati wa Kikao cha tathmini ya
utendaji kazi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi
kilichofanyika Ukumbi wa Mwalimu Nyerere jijini Dar es Salaam.
Mgaya ameeleza kuwa, ujio wa sheria
ya Ajira na Mahusiano Kazini Na. 6/2004 pamoja na Sheria ya Taasisi za Kazi Na.
7/2007 zimesaidia kuleta mabadiliko makubwa katika Nyanja za utoaji haki.
“Kupitia Mpango wa Matokeo Makubwa
Sasa (BRN) yapo maeneo ya Sheria za Kazi ambayo kama wadau tunadhani ni lazima
kufanya mabadiliko yenye tija kwa lengo la kurahisisha utendaji kazi wa
Mahakama hii ya Kazi ili haki ya kila upande iweze kupatikana kwa wakati”,
alisema Mgaya.
Aidha, Mgaya amegusia baadhi ya
changamoto zinazokwamisha katika kupata haki katika Mahakama ya Kazi ikiwemo
uhaba wa Majaji na Wasajili katika Mahakama, Upotevu wa Mafaili, Uhamisho wa
Majaji, Madalali wa Mahakama, Kukinzana kwa Maamuzi ya Mahakama pamoja na
Upungufu wa vitendea kazi.
Naye Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri
Mkuu anayeshughulikia Watu wenye Ulemavu Mhe. Abdallah Possi ameeleza kuwa Mahakama
sio chombo cha kutafsiri sheria na kutoa haki tu, bali ni chombo pia cha kukuza
uchumi.
“Mahakama inavyotatua migogoro
inasababisha hali ya utulivu katika sehemu za kazi kwa sababu uchumi wa nchi
hauwezi ukakua kama zile sehemu za uzalishaji zitakua na migogoro.”Alisema
Possi.
Akiongea kuhusu masuala ya watu wenye
ulemavu, Mhe. Possi alisema kuwa Sheria za Kazi nchini zinakataza masuala ya
unyanyapaa wa aina yoyote, hivyo Waajiri pamoja na Vyama vya Wafanyakazi
havinabudi kuzingatia usawa kwa watu wenye ulemavu.
Kwa upande wake Jaji Mfawidhi wa
Mahakama Kuu, Divisheni ya Kazi, Mhe. Aisha Nyerere amesema kuwa, Mahakama ya
Kazi ina wajibu wa kutolea maamuzi mashauri ya kikazi yaliyofunguliwa.
Aidha, ameongeza kuwa Kanuni ya saba Kanuni
ndogo ya Kwanza ya Tangazo la Serikali la 2009/2010 linaelekeza kuundwa kwa Kamati
ya Utatu katika Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi ambapo kamati hizo zinaundwa na
Jaji, Msajili katika Mahakama ya kazi, Mwanasheria wa Serikali Mfawidhi au Mwakilishi
wake, Wajumbe wawili katika Vyama vya Wafanyakazi, Wajumbe wawili kutoka Vyama
vya Waajiri, Mawakili wawili kutoka Chama cha Mawakili wa Tanganyika na
Kamishna wa Kazi.
Kikao cha Tathmini ya Utendaji kazi
wa Mahakama Kuu, Divisheni ya Kazi kilichofanyika leo kimeshirikisha wadau mbalimbali wa Sheria wakiwemo
Majaji,Mawakili,Wasajili, Wenyeviti wa Vyama vya Wafanyakazi na Vyama vya
Waajiri.
0 comments:
Post a Comment