Pages

Ads 468x60px

Tuesday, August 29, 2017

MADIWANI RUNGWE WASUSIA POSHO, WADAI MALIMBIKIZO YA MIEZI MINNE YA POSHO YA MWEZI


 Na Moses Ng’wat, Rungwe.

 MADIWANI wa Halmashauri ya Rungwe
 wamesusia posho ya kikao cha kupitia na kujibu hoja za
 Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu (CAG ) kwa madai kuwa
 Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri hiyo, Loema Peter,
 amezipunguza bila kuwafahamisha.
 Madiwani hao 38  wamegomea posho
 ya shilingi  100000  wakitaka kulipwa posho ya
 awali shilingi 150,000, huku wakilalamikia kutolipwa
 malimbikizo ya posho ya mwezi ambayo hawajalipwa kwa miezi
 minne.

 Tukio hilo lilitokea muda mfupi baada
 ya kikao hicho kilichosimamiwa na Mkuu wa Mkoa, Amos
 Makalla, kumalizika ambapo madiwani hali walikataa kusaini
 kiasi hicho wakidai ni pungufu tofauti na walivyokuwa
wakilipwa awali.

 Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo, Ezekiel
 Mwakota, alikiri kususia posho hiyo , huku akisisitiza ni
 haki ya Madiwani kwa kuwa hawakupewa taarifa kama kuna
mabadiliko katika utaratibu mpya wa malipo ya posho za
 Madiwani.
 
 “Suala hilo linajadiliwa kwenye
 vikao, ni haki yao Madiwani kutochukua kiasi hicho cha fedha
 kwani hawakuwa na taarifa yeyote ya mabadiliko, lakini
 ukweli ni kwamba kuna mabadiliko posho za Madiwani
 wanahitaji ufafanuzi”.
 Mwakota aliongeza kuwa, Madiwani
 wanalipwa posho ya mwezi kutokana na makusanyo ya mapato ya
 ndani, hivyo kwa kipindi cha miezi mitatu wameshindwa
 kulipwa kutokana na kusuasua kwa ukusanyaji.
 “Ni kawaida jambo hili hapa Rungwe ni
 la muda mrefu na ni kama utaratibu tuliojiwekea kuwa,
 Madiwani wawe wa mwisho kulipwa…huwezi kulipa Madiwani
 kwanza wakati kuna watendaji wengi hawajalipwa”.
 Aliongeza kuwa suala hilo linaendelea
 kujadiliwa na Madiwani hao watalipwa madai yao yote ndani ya
 muda mfupi, hasa kwa fedha za mwezi Mei na Juni kwa kuwa
 mchakato wa fedha hizo tayari umefikia hatua nzuri.

 Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri
 hiyo, Loema alipoulizwa juu ya tukio hilo hakuwa tayari
 kulizungumzia na kusema suala hilo halijafika kwake.
Mwisho.

0 comments:

Post a Comment