Pages

Ads 468x60px

Tuesday, August 28, 2012


MKUU wa Wilaya ya Mbozi, Mkoani, Dk. Michael Kadeghe, amesema kuwa asilimia 75 ya fedha zinazokusanywa katika kodi na vyanzo vingine mbalimbali vya mapato katika halmashauri hiyo huishia mifukoni mwa watendaji wa vijiji, kata na baadhi ya watumishi wa serikali wenye wajibu wa kusimamia kazi hiyo.
Alitoa kauli hiyo jana wilayani hapa, wakati akitoa hotuba ya ufunguzi ya mdahalo ulioandaliwa na Mtandao wa Asasi zisizo za serikali wilaya ya Mbozi (MNN) na kufanyika katika ukumbi wa Mkonongo.
Lengo la mdahalo huo ni kuimarisha ushirikiano , uwajibikaji na uwazi kati ya wabunge/madiwani , viongozi wa serikali na wananchi katika kufuatilia kero na mahitaji ya huduma za jamii.
 Dk. Kadeghe alisema kuwa baada ya kutembelea katika vijiji mbalimbali wilayani humo kwa lengo la kusikiliza kero mbalimbali, imebainika kuwa sehemu kubwa ya malalamiko ya wananchi yanahusu ufujwaji wa fedha za umma.
Alisema mbali na ubadhilifu huo alioubaini, lakini pia asilimia kubwa ya watendaji hao wa vijiji na kata wamekuwa wakivunja sheria kwa kushindwa kusoma mapato na matumizi, hali ambayo imesababisha wananchi wengi kujenga chuki na serikali.
Pia alisema watendaji hao wamefikia hatua hiyo ya kufuja kiasi hicho kikubwa cha makusanyo hayo kwa asilimia 75 bila kuchukuliwa hatua za kisheria kutokana na wengi wao kushirikiana na baadhi ya wakuu wa vitengo katika Halmashauri hiyo.
Alisema kutokana na hali hiyo ameamua kuingia vitani ili kupambana na wezi hao na kwa kuanzia , atawashughulikia wale wote waliohusika katika ufisadi wa fedha zilizotengwa katika miradi ya uchimbaji wa mabwawa.
Katika kuhakikisha kuwa yuko tayari kupambana na vitendo hivyo vichafu ,Mkuu huyo wa wilaya aliamua kutoa namba yake simu ya mkononi  0713-622750 kwa wananchi ili waweze kutoa taarifa wakati wowote pindi wananchi wanapobaini kufanyika kwa vitendo hivyo.
Kwa upande wake mtoa mada kutoka asasi ya Wadf-Mbozi, Happness Kwilabya, alishauri kuundwa na kuanzishwa kwa chombo maalumu ambacho kitatoa nafasi kwa wapiga kura kukaa pamoja na viongozi waliowachagua ili kujadili na kupeana mikakati ya kuendesha jimbo lao, badala ya utaratibu wa sasa wa kutumia mikutano ya hadhara ambayo wananchi hawapewi nafasi ya kujadiliana na mwakilishi wao.
Alisema hali hiyo kwa muda mrefu imesababisha kuwepo kwa changamoto kubwa ya uhusiano kati ya makundi hayo na kusababisha kuendelea kudorora kwa  michakato ya shughuli za maendeleo na maendeleo kwa ujumla wilayani hapa.
Naye Neckwell Kitta, kutoka asasi ya kujitolea ya masuala ya afya wilaya ya Mbozi (MBOHECO) akieleza wajibu wa raia katika mchakato wa maendeleo, alisema ni lazima kila mtu kufanya kazi  kwa kujituma na uaminifu mkubwa kwa  kuwa kazi ndio huzaa utajiri wa mali katika jamii na ndio chimbuko la ustawi wa jamii.
Aliongeza kuwa kama kila mtu atajituma kwa uaminifu katika kazi halali za uzalishaji mali , kwa kutimiza nidhamu ya kazi anaweza kufikia malengo ya binafsi na yale ya pamoja yanayotakiwa na kupangwa kwa mujibu wa sheria.
Kwa upande wa asasi za kiraia, alisema lengo kuu ni kuielimisha jamii kuhusu wajibu wa kiraia,kisiasa na kisheria, pamoja na kuwezesha jamii na makundi yaliyosahaulika kushiriki kikamilifu katika mchakato wa demokrasia na kufanya maamuzi.

Mwisho.

0 comments:

Post a Comment